MISWADA MITATU YAWASILISHWA ILI KUJADILIWA KWA KINA BUNGENI KUANZIA LEO

Na, Mwandishi Wetu - Dodoma

Mapema Leo Bunge la Tanzania limeanza rasmi vikao vyake Jijini Dodoma ambapo Vikao hivyo vinatarajiwa kudumu kwa muda wa wiki tatu kwa ajili ya kujadili kwa kina mapendekezo yaliyowasilishwa na wadau mbalimbali katika miswada mitatu.
Bunge likisikiliza Miswada iliyowasilishwa bungeni leo Januari 30, 2024 Bungeni Jijini Dodoma.

 Miswada hiyo iliyowasilishwa bungeni hapo ni Muswada wa Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge, na Madiwani wa Mwaka 2023, Muswada wa Sheria ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi wa Mwaka 2023 na, Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria za Vyama vya Siasa mwaka 2023 hii ikiwa ni baada ya kuwasilishwa katika Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria ambapo, kwa muda wa siku nne mfululizo, kamati ilipokea maoni kutoka kwa zaidi ya taasisi elfu moja na inatajadiliwa bungeni hapo.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. Jenister Mhagama na Mwenyekiti wa kamati hiyo Dkt. Joseph Mhagama wameiwasilisha bungeni hapo ambapo pamoja na mambo mengine Mwenyekiti huyo amebainisha maoni yaliyotolewa ikiwa ni pamoja na kutaka wakurugenzi wa halmashauri kuondolewa mamlaka ya kusimamia uchaguzi.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Mhe. Jenister Mhagama wakati akiwasilisha muswada bungeni leo January 30, 2024.

Aidha pendekezo lingine ni la kutaka kuondolewa kwa takwa la ushindi wa kura za urais kuwa zaidi ya asilimia 50, pamoja na kuondolewa kwa gharama za kuchukua fomu kwa wagombea, baadhi ya wadau pia wametaka vyama kulazimishwa kuteua asilimia 50 ya wagombea wanawake kwa lengo la kuleta uwiano wa kijinsia katika nyanja mbalimbali za kisiasa.

Ikumbukwe kuwa hii inakuja baada ya Minong'ono na Shinikizo la wadau mbalimbali na vyama pinzani kutaka Katiba Mpya hasa kipindi hiki ambacho Taifa linajiandaa kuelekea uchaguzi wa serikali za mitaa, na baadae 2025 kwa uchaguzi mkuu.

Hata hivyo Miswada hiyo inatokana na maoni yaliyopendekezwa na wadau, ikiwemo vyama 17 vya kisiasa, asasi za kiraia, viongozi wa dini na wanaharakati wengine. 

Mwenyekiti wa kamati hiyo Dkt. Joseph Mhagama wakati akiwasilisha muswada Leo Januari 30, 2024 Bungeni Jijini Dodoma.

Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Tulia Ackson akiendesha Bunge Leo Januari 30, 2024 jijini Dodoma

 








Je?, UNA HABARI,PICHA, TANGAZO AU TAARIFA AMBAYO UNGEPENDA TUICHAPISHE KATIKA MTANDAO HUU? WASILIANA NASI, Email : fichuziblog@gmail.com , Simu +255 752 925 603

0 Comments

Post a Comment

Post a Comment (0)

Previous Post Next Post

TUTUMIE UJUMBE HAPA